IQNA

Wapalestina wakumbwa na maafa mengine katika kumbukumbu ya Siku ya Nakba

13:18 - May 16, 2018
Habari ID: 3471515
TEHRAN (IQNA) -Utawala dhalimu wa Israel umewaua kwa umati Wapalestina sambamba na hatua iliyo kinyume cha sheria za kufunguliwa ubalozi wa utawala wa Marekani katika mji wa Quds (Jerusalem).

Matukio hayo mawili chungu yamejiri sambmba na mwaka wa 70 tangu siku ilipoanza kukaliwa kwa mabavu Palestina ambayo ni maarufu kama Siku ya Nakba yaani Siku ya Maafa na hivyo kuwadhihirishia walimwengu jinsi wananchi Wapalestina wasio na ulinzi wanavyodhulumiwa.

Taarifa za karibuni kabisa zinaonyesha kuwa, juzi Jumatatu Wapalestina 59 waliuawa shahidi katika Ukanda wa Gaza na wengine 2771 walijeruhiwa kufuatia mashambulio na ufyatuaji risasi uliofanywa na wanajeshi wa Kizayuni dhidi yao. Hii ni katika hali ambayo, kwa majuma kadhaa sasa jinai za utawala wa Kizayuni wa Israel dhidi ya Wapalestina zimeshadidi na kupelekea kumwagwa damu za maelfu ya Wapalestina.

Matukio ya Palestina katika kumbukumbu ya maafa ya mwaka wa 70 wa kukaliwa kwa mabavu ardhi hiyo yanaonyesha kuwa, masaibu ya Wapalestina yanayotokana na jinai za Israel na waungaji mkono wake wa Kimagharibi si tu hayana kikomo wala mwisho, bali yamekuwa yakichukua mkondo mpana zaidi siku baada ya siku na kuwafanya wananchi hao wakabiliwe na misiba mikubwa zaidi.

Neno 'Nakba' linakumbusha mambo mawili mabaya mno katika kumbukumbu za Wapalestina na fikra za waliowengi. Mosi, ni kuundwa utawala ghasibu wa Israel mwaka 1948 na pili kufukuzwa zaidi ya Wapalestina laki nane katika ardhi yao ya asili ambapo filihali idadi ya wakimbizi wa Kipalestina imefikia milioni sita.

Siku ya Nakba si nembo ya maafa tu yaliyotokea katika mwaka huo katika ardhi ya Palestina, bali ni dhihirisho la matatizo na masaibu liliyotwishwa taifa hilo katika kipindi cha miongo kadhaa iliyopita.

Ukweli wa mambo ni kuwa, Yawm an-Nakba (Siku ya Nakba) ni simulizi ya mauaji ya kizazi ambayo ilifuatiwa na kuharibiwa sehemu kubwa ya misingi ya kisiasa, kiuchumi, kiutamaduni na haki za Wapalestina ili kuandaa uwanja na kufungua njia ya kutangazwa uwepo wa utawala mmoja bandia na haramu.

Kubomolewa zaidi ya miji na vijiji 675, kukaliwa kwa mabavu maeneo ya Wapalestina na kubadilishwa kuwa vitongoji vya walowezi wa Kiyahudi, kutimuliwa Wapalestina, kuangamizwa turathi na athari za utambulisho wa kitaifa wa Palestina na kuondolewa majina ya Kiarabu na badala yake kupachikwa majina ya Kiibrania ni miongoni mwa hatua zilizochukuliwa na utawala wa Kizayuni wa Israel kuanzia 1948 hadi sasa.

Siku ya Nakba inaashiria pia makumi ya matukio ya mauaji ya umati na jinai za kutisha za Israel ambapo katika matukio hayo ya kinyama maelfu ya wanawake na watoto wa Kipalestina waliuawa kikatili.

Katika uga huo tunaweza kuashiria mauaji ya kimbari ya utawala wa Kizayuni wa Israel huko Kafr Qasim na Deir Yassin. Tarehe 29 Oktoba 1956 Wapalestina 48 wakiwemo wanawake 6 na watoto 23 waliuawa kinyama na bila sababu katika kijiji cha Kafr Qasim katika Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan. Kabla ya jinai hiyo,  yaani tarehe 9 Aprili 1948 pia, makundi mawili ya kigaidi ya Wazayuni ya Irgun na Lehi (stern) yalikivamia kijiji cha Deir Yassin magharibi mwa Quds inayokaliwa kwa mabavu na kuwaua kwa umati wakazi wake 360 wasio na ulinzi.

Tab'an, tangu utawala wa bandia wa Israel uasisiwe, hakuna wowote ambapo jinai zake pamoja na hatua zake za kupenda kujitanua katika ardhi za Palestina zimewahi kusita; na mfano wa karibuni kabisa ambao tunaweza kuuashiria ni mauaji na jinai ya juzi Jumatatu huko Palestina ambayo imetekelezwa kwa ridhaa na baraka za Marekani.

Gazeti la al-Quds al-Arabi linalochapishwa London Uingereza limeandika katika ukurasa wake mtandao wa Intaneti kwamba: Kufunguliwa ubalozi wa Marekani katika mji wa Quds ni nakba na msiba mpya kwa taifa la Palestina, uadilifu na uhalali wa kisheria kimataifa.

3465848

captcha