IQNA

Wageni 20,000 katika Sherehe za Maulid ya Mtume SAW kisiwani Lamu, Kenya

14:47 - December 12, 2017
Habari ID: 3471307
TEHRAN (IQNA)-Zaidi ya wageni 20,000 kutoka kote duniani wanahudhuria sherehe za Maulid ya Mtume SAW inayofanyika katika Kisiwa cha Lamu katika Pwani ya Kenya.

Katibu Mwandalizi wa Sherehe za Maulid mjini Lamu, Ustadh Idarus Muhsin ameliambia gazeti la Daily Nation kuwa wageni wa kitaifa na kimataifa wanaendelea kuwasili kwa ajili ya sherehe hizo za kila mwaka.

Aidha amesema sherehe hizo zitaendelea kwa muda wa siku nne wiki hii kuanzia Jumanne hadi Ijumaa katika Mji wa Kale wa Lamu ambao uko katika orodha ya UNESCO ya Turathi za Dunia.

Ustadh Muhsin ameongeza kuwa, wageni wa kimataifa ni kutoka nchi kama vile Tanzania, Yemen, Oman, Visiwa vya Komoro, Umoja wa Falme za Kiarabu, Uingereza na maeneo mengine duniani.

"Tunataraji wageni baina ya 15,000 hadi 20,000 katika sherehe za Maulidi mwaka huu.

Naye mratibu wa Sherehe za Maulidi mjini Lamu Sheikh Mohamed Khitamy wa Msikiti wa Riyadha amesema Maulidi ya mwaka huu ni ya 130 tokea sherehe hizo zianzishwe mjini humo.

Wakati huo huo Kamishna wa Kaunti ya Lam Gilbert Kitiyo amesema usalama umeimarisha kote Lamu na kwamba magari yote yanayoingia na kuondoka kaunti hiyo yatafanyikwa ukaguzi mkali. Amewahakikishia washiriki wote wa sherehe za Maulidi kuwa watakuwa katika eneo salama. Eneo hilo limekuwa likikumbwa na hujuma za magaidi wakufurishaji mara kwa mara.

Mji wa Lamu ni kati ya miji ya kale zaidi katika mwambao wa Afrika Mashariki na ni turathi muhimu ya Uislamu na ustaarabu wa Waswahili.

3671805

captcha