IQNA

Shirika la Binladin laondolewa lawamani baada ya kuanguka winchi Makka

15:22 - October 03, 2017
Habari ID: 3471203
TEHRAN (IQNA)-Mahakama moja nchini Saudi Arabia imesema Shirika la Ujenzi la Binladin halina hatia na haliwezi kubebeshwa dhima ya kuanguka winchi (crane) katika Msikiti Mtakatifu wa Makka wakati wa msimu wa Hija mwaka 2015.
Shirika la Binladin laondolewa lawamani  baada ya kuanguka winchi MakkaMahakama ya Saudi imeliondoa shirika la Binladin lawamani Jumatatu baada ya shirika hilo kujitetea kwa kusema kuwa, halingeweza kutabiri upepo mkali uliopelekea kuanguka winchi.

Ikumbukwe kuwa mnamo Septemba 11 mwaka 2015, winchi kubwa ya ujenzi ilianguka katika Msikiti Mtakatifu wa Makka na kuwaua watu 100 na kuwajeruhi wengine 200 kabla ya kuanza Ibada ya Hija.

Shirika hilo linamilikiwa na familia ya Bin Laden, ambayo ina uhusiano wa karibu na ukoo wa Aal Saud unaotawala Saudi Arabia. Binladin linatambulika kama shirika la pili kwa ukubwa la ujenzi duniani baada ya Shirika la Ujenzi la Vinci la Ufaransa. Binladin lina makao yake mjini Jeddah na ilianzishwa mwaka 1931 na Sheikh Mohammed bin Laden, baba yake Osama bin Ladin kinara aliyeuawa wa kundi la kigaidi la al Qaeda. Inadaiwa kuwa Osama alikanwa na familia yake katika muongo wa 90.

Kwa mujibu wa tovuti ya Shirika la Ujenzi la Binladin, shirika hilo limehusika katika ujenzi wa miradi muhimu Saudia kama vile jingo la al-Faisalia mjini Riyadh, Kituo cha Kifedha cha Mfalme Abdullah, vyuo vikuu kadhaa na Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mfalme Abdul Aziz mjini Jeddah.

3464067

captcha